WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema nchi haijakumbwa na baa la njaa na amewataka Watanzania utosikiliza kampeni za upotoshwaji zinazofanywa na baadhi ya wafanyabiasha kuhusu hali ya chakula kwani si za kweli bali ni za uzushi zenye lengo la  kupandisha bei za vyakula.
Amesema Serikali ndio yenye jukumu la kutoa taarifa za kuwepo kwa njaa ama kutokuwepo na kwamba taarifa zinazosambazwa za kuwepo kwa baa la njaa nchini hazina ukweli wowote na Serikali inawahakikishia wananchi kuwepo kwa usalama wa chakula.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo jana 
Jumatatu, Januari 16, 2017 wakati akizungumza na waandishi wa habari mkoani hapa mara baada ya kuzindua safari za ndege za Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kutoka Dar es Salaam kwenda Dodoma, ambapo amesisitiza kwamba hali ya upatikanaji chakula nchini ni tofauti na inavyoelezwa na baadhi ya vyombo vya habari.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo baada ya kutolewa kwa taarifa katika vyombo mbalimbali vya habari kuhusu kuwepo kwa baa la njaa nchini jambo ambalo amesisitiza kuwa si la kweli. Amewataka wananchi kuwa watulivu na jambo hilo likitokea Serikali itatoa taarifa.
“Mwaka jana nchi ilikuwa na akiba ya chakula cha zaidi ya tani milioni tatu hali iliyopelekea baadhi ya Wabunge na wafanyabiashara kuomba kibali cha kuuza nafaka nje ya nchi, ambapo Serikali ilitoa kibali hicho baada ya kujiridhisha kuwepo kwa akiba ya kutosha ya chakula,” amesema.

Amesema baada ya kutolewa kwa kibali hicho tani milioni 1.5 ziliuzwa nje ya nchi na Kiasi cha tani milioni 1.5 zilizobaki zilihifadhiwa kama akiba ambapo tayari wameruhusu ziuzwe hapa nchini ili kupunguza kupanda kwa bei za vyakula nchini.
“Naomba wananchi msiwe na wasiwasi juu ya hali ya chakula nchini. Msisikilize kelele zinazopigwa na watu mbalimbali pamoja kwenye baadhi ya vyombo vya habari yakiwemo magazeti kwani taarifa hizo si za kweli. Chakula kipo cha kutosha licha ya mvua kusuasua katika baadhi ya maeneo nchini,” amesema.
Hata hivyo Waziri Mkuu amesema kuwa kwa sasa mvua zimeanza kunyesha katika maeneo mbalimbali nchini, hivyo amewaomba wananchi kuzitumia kwa kulima mazao ya muda mfupi yanayostahimili ukame.

Waziri Mkuu amesema kwamba endapo kutatokea uhaba wa chakula nchini, Serikali itatoa utaratibu wa namna ya upatikanaji wa chakula kwa wananchi wake. Kuhusu kupanda wa bei ya vyakula katika baadhi ya masoko amesema inatokana na kuwepo kwa uhaba wa chakula katika nchi jirani.
Aidha, Waziri Mkuu amesema kwamba Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, itatoa taarifa kuhusiana na hali halisi ya chakula nchini kwa sasa na pia itatoa taarifa kuhusu hali ya mvua ili Watanzania waweze kupata ukweli wa hali ilivyo.

Waziri Mkuu Mhe  Kassim Majaliwa akizungumza wakati alipozindua safari za ndege za Shirika la Ndege la Tanzania kati ya uwanja wa Julius Kambarage Nyerere na Dodoma katika hafla iliyofanyika kwenye uwanja wa ndege wa Dodoma Jana.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...